Nguvu Za Giza

Kutambua Mbinu za Shetani kwa Kutumia Mwanga wa Neno la Mungu.

Lengo la Biblia Takatifu silo kuangalia hasa Shetani na kazi zake. Japokuwa tunapata mengi kwenye Biblia yanayofunua tabia zake na kazi zake.

Wakati fulani Shetani alikuwa malaika, lakini aligeuka kinyume cha Mungu, Muumba wake, na akatamani kuwa kama Mungu. Matendo ya ufalme wa giza wa Shetani siyo mageni. Yanaonyesha dhahiri jitihada za Shetani kwa miaka kupingana na Ufalme wa Mungu. Anatoa mbadala wa kile ambacho Mungu anatimiliza kwa kupitia nguvu za Roho Mtakatifu.

Twasoma katika kitabu cha Kutoka juu ya nguvu ya walozi wa Misri waliojaribu kufanya miujiza Mungu aliyofanya kwa mkono wa Musa. Na kwenye kitabu cha Ayubu, Shetani anadhihirishwa kama mwenye wivu sana juu ya uaminifu wa Ayubu kwake Mungu. Alitumia ukatili na unyang’anyi ili ajaribu kumlazimisha Ayubu kwenda kinyume na Mungu.

Njia za shetani zinatambuliwa na: Woga, vitisho, ahadi za kupata anasa na nguvu, misukumo, mashaka, na tuhuma. Baadhi ya mambo ya kwanza anayoyatambulisha kwetu yanaonekana ni ya kuvutia sana na ya kusisimua. Anashauri, “Ungependa kujua mambo ya mbeleni au kuwa na ufahamu ambao wengine hawawezi kuwa nao?” Anaweza kukupa uponyaji ambao uko nje ya idara ya kisayansi. Utabiri wa mambo yajayo huenda unaonekana kwamba hauna madhara wala ubaya, lakini unafuatwa na mengine ya uchawi wa macho, pamoja na kutumia dawa za kienyeji na uchawi wa kumroga mtu, na hatimaye kumpelekea mautini. Wazo linaanza kutuingilia kuwa kuna baadhi ya roho za kuheshimiwa na kuogopwa kwa sababu ya nguvu zilizo nazo juu yetu. Kwa hiyo, Shetani anawanasa hao wasiokuwa waangalifu kwenye mtego wake wa kuendeshwa na woga kwake na roho zake.

Watu wengi sana wamekamatwa na shauku ya vitu ambavyo, kwa mara ya kwanza vilionekana kuwa vyema. Kwa kufanya majaribio ya utabiri wa mambo yajayo na uchawi wa aina mbalimbali, watu wanajiweka kwenye mazingira hatarishi ya kusumbuliwa zaidi na mapepo ya giza.

Lengo la shetani ni kumomonyoa na hatimaye kuharibu imani ya mkristo kwa Mungu. Mkristo apata ushindi kwa kuwa na imani kwa Yesu Kristo peke yake. Wakati mwingine hamu ya kujua visivyojulikana au matamanio ya nguvu vinamsukuma mtu afanye majaribio na hayo ambayo ni ya ufalme wa Shetani. Imani ya kukaza kwa Mungu humpumzisha mtu asivutiwe na yale yasiyojulikana na pia inamimarisha kabisa katika nguvu za Kristo.

Maandiko kamili ya: Nguvu Za Giza

Yale yaliyoanza kutokana na shauku au majaribio punde yanamnasa mtu kwenye wavu wa hofu, hofu ya kile kinachoweza kutokea mbeleni, hofu ya nguvu kuu, hofu ya watu wengine, hofu ya Shetani mwenyewe. Hizi hofu zinamfunga mtu aliyeruhusu mwenyewe kujihusisha na matendo yasiyo na uhakika. Kutibu hofu hii, Shetani anadai kuwa anao dawa nzuri: Eti atatoa nguvu zaidi kama mtu atajisalimishia utaratibu fulani au kutii amri kadhaa. Shetani asema kwamba hofu ya roho nyingine zinaweza zikashindwa kwa kujipatia nguvu kubwa zaidi kwetu wenyewe. Kwa hiyo mtu anaingizwa kwenye hatua za kufikia nguvu zaidi ambazo, badala ya kumpandisha kwenye kiwango cha juu cha amani, zinamzamisha chini katika kina kirefu cha machukizo ya kishetani. Usalama ulioahidiwa na shetani hauonekani, na hubadilishwa kwa uhitaji wa kulindwa na nguvu zilizo juu zaidi kwenye huu ufalme wa uovu. Huu ndio mfumo wa kishetani.

Mpango wa shetani ni kumzidi Mungu. Shetani aliumbwa kuabudu, na sio kuabudiwa. Yeye sio nguvu ya juu; hawezi kumzidi Mwana Kondoo wa Mungu; hawezi kutoa amani; hana nia na ushindi wetu. Hata hivyo anaendelea na kazi ya kuwatawala watu ili watu wamtumikie yeye. Anajaribu kuleta mashaka kuhusu Mungu na ufalme wake. Anajitahidi kuanzisha taasisi yake na yeye akiwa kama mfalme. Hii inaendelezwa kwa utaratibu wa hofu na udanganyifu wa nguvu. Anafanya miujiza ili awashangaze na kushawishi watu kusudi awawekee kifungo akilini mwao (2Wakorintho 11:14,15). Madhara ya mtego huu ni kuharibu amani na usalama kwa watu binafsi, majumbani, na hata serikalini. Hio inawakamata watu, na inasababisha wajisikie kutishwa sana kama watajaribu kutorokea ufalme huo.

Shetani ni mkali sana, mchoyo sana, mkatili sana, adui mbaya sana uliye naye wewe. Yeye hana heshima hata kidogo. Yeye ni mwongo. Hakuna ukweli ndani yake- “Yeye ni mwongo, na ni baba wa huo [uongo]” (Yohana 8:44). Yeye ni muuaji, mharibifu. Yeye ni mfano wa chuki na uovu. Yeye ni mwovu kabisa ambaye hana uzuri uliobakia kwake!

Shetani ni mchochezi wa maovu yote. Hakuna kosa wala dhambi ambayo kwake ni ovu sana au chafu sana kwake. Yeye ni chanzo cha chuki zote, mauaji yote, kila aina ya kutesa watoto au kupiga wanawake, kila aina ya madawa ya kulevya, kila aina ya uzinzi, ndoa zote zilizovunjika, kila aina ya kutokuelewana, kila uchawi, kila kutokuwa na uaminifu. Anafurahi kusababisha hamu ya kuvunja sheria na uovu, uvunjaji wa sheria unaofanyika juu ya watu wengine wema ambao, kwa bahati mbaya, wanaangukia mikononi mwa wasio haki na wapotovu. Yeye ni mkatili na hana msamaha. Hana huruma kwa hao wanaopata mateso. Kumwaga damu na vifo ndio silaha anazotumia kutekeleza kazi zake. Amekuja “kuiba, kuua, na kuharibu” (Yohana 10:10).

Mwisho wa milele wa Shetani ulishaamulika. Kuna sehemu ya moto wa milele ilishaandaliwa kwa ajili yake na malaika wake (Mathayo 25:41). Anajishughulisha na kupata watu wengi kadiri atakavyoweza ili wapate hayo mateso pamoja naye. Anajua anaweza kufanya hivi kwa kuimomonyosha, kuidhoofisha, na mwishowe kuiangamiza imani yetu kwa Mungu. Atafanya hivi kwa kulipinga Neno la Mungu kwa uwazi, ama kwa ujanja na werevu anawahamasisha “wakristo” walio vugu vugu, wasiojali, na waliokubali Ukristo usio na masharti.

Kuna ukombozi kutoka kwenye umiliki na utumwa wa Shetani. Atakufanya uamini ya kuwa hakuna njia ya kutoka. Biblia inatuambia ya kwamba Yesu alikuja kuwaweka huru waliotekwa mateka. Amekuja kuleta uzima. Yesu ni njia, kweli, na uzima (Yohana 14:6). Wakati alipokuwa hapa duniani, Yesu alionyesha nguvu zake juu ya Shetani kwa kushindana na majaribu ya Shetani na akitupa nje nguvu za giza kwa kutumia Neno la Mungu (Mathayo 4:1-11; Marko 9:25,26). Yesu alishinda nguvu za Shetani kwa kifo chake msalabani na kufufuka kwake kutoka wafu.

Je, tunawezaje kujumuishwa katika ushindi huo wa kumzidi huyu adui mkuu wa nafsi zetu? Kwanza, lazima tufahamu ya kwamba tulikuwa tumetekwa na shetani na kufungwa na hofu yake. Lazima tukubali kwamba huku ni hali ya dhambi na kwamba tumepotea tukibakia hali hii. Tunapogundua hili kwamba hatuwezi kujiokoa wenyewe kutoka mkononi mwa Shetani, lazima tumlilie Mungu ukombozi wake kwa moyo wetu wote. Lazima tuzitubu na kuziacha dhambi zetu. Twahitaji kukubali kwa imani, damu ya Yesu Kristo yenye utakaso kwa ajili ya dhambi zetu. Lazima tujitoe nafsi zetu kwa Mungu, kukubali msamaha wake na kwa uaminifu kutii Neno lake. Tunapotimiza haya masharti, anatupa amani kwake, anayatuliza mahangaiko mioyoni mwetu, anasamehe dhambi zetu, anatufanya kuwa kiumbe kipya na kutufanya mmoja wa wanawe. Hii ndio inamaanisha kuzaliwa upya. Yeyote anayepinga mwito wa Mungu bado yumo katika ufalme wa Shetani, na mwishowe, mdanganyi atampeleka huyo mtu pamoja naye kwenye mateso ya milele.

Kama huelewi mpango ambao Mungu amekuwekea, jifunze Neno la Mungu, na umwombe Yeye kwa uaminifu moyoni, na atakuonyesha njia. Mungu anakuita kwake na anataka wewe utoroke na utumwa wa Shetani. Mungu akubariki. Soma Zaburi 91.

Masomo Mengine:

Luka 11:20-23 Mmoja mwenye nguvu zaidi ya Shetani

Warumi 6:20-23 Kuwa huru kutoka kwenye dhambi

Isaya 61:1 Kuwekwa huru mateka

Warumi 8:1,2 Kuwa huru na laana na hatia

Mawasiliano

Kuagiza Vipeperushi

Je, Wewe Ni Mwaminifu Kwa Kiasi Gani?

Tazama wapendezwa na kweli iliyo moyoni” (Zaburi 51:6).

Uaminifu ni maadili ya ukweli katika kufungamana na mambo yote ya maisha. Kwa hakika uaminifu ni jambo la moyoni, pia ni fundisho la msingi la Injili ya Yesu Kristo. Mungu anajua mawazo na makusudi ya moyo. Anatambua ukweli kama msingi muhimu kwa maana yeye ni Mungu wa ukweli. (Kumb. 32:4) Hakika atabariki uaminifu uliokamilika wa moyo wetu.

Je, unao tabia ya kusema ukweli wakati ungeweza kupatikana na jambo, lakini ukawa si mwaminifu wakati ambao hakuna atakayekugundua?

Je, kwa makusudi unaweza kumridhisha mtu kwa ushawishi usio wa kweli?

Je, unaweza kufanya manunuzi kwa kukopa wakati ulifahamu kwamba huna uwezo wa kulipa?

Je, unamwambia Mungu jinsi mambo yalivyo wakati unapomwomba?

Je, kwa uaminifu unalitenda kila jambo ambalo unafahamu Mungu anakutaka ulitende?

Maandiko kamili ya: Je, Wewe Ni Mwaminifu Kwa Kiasi Gani?

Je, wewe ni mwaminifu kuhusu mafundisho ya Biblia?

Je, jinsi unavyojifanya kuonekana, kweli ndivyo ulivyo?

Kuna hadithi ya kuchochea hisia katika Agano Jipya ya mtu aitwaye Anania na mkewe Safira katika kitabu cha Matendo 5:1-11. Waliuza mali yao kama wengine nao walivyofanya na kujifanya kutoa fungu lote kwa kanisa, wakati kwa hila walikubaliana kubakiza sehemu ya malipo kwa ajili yao. Anania na Safira walileta pesa hizi mbele ya viongozi wa kanisa wakisema kwamba waliuza shamba hilo kwa kiasi hicho walicholeta. Udanganyifu wao ulihukumiwa na Mungu mara moja na kuadhibishwa kwa kifo. Katika habari hii ya kanisa la mwanzo, unafiki (au udanganyifu) ulikuwa ukiadhibishwa kwa ukali. Mungu hapuuzi uzushi huu. Nasi kama Anania na Safira huenda tunaweza tukatoa uzushi unaoridhisha hata kama maneno tuyasemayo siyo ya uongo. Twaelekea kusahau uwajibikaji wetu mbele za Mungu. Mungu ajua jinsi mioyo yetu ilivyo, na anatutegemea tuwe waaminifu na wa kwelikweli.

Mnafiki hujifanya kuwa mtu ambaye siye yeye. Huenda anadai kuwa mwaminifu, lakini wakati ambao ingekuwa manufaa kwake, yuko tayari kusema uongo. Labda anaweza kuzungumzia vizuri kuhusu mahitaji ya wasiobahatika, lakini siye mkarimu wa kutoa muda wala msaada wakati maafa au matatizo yakitokea. Mtu mwingine aweza kujifanya kuwa mkarimu kujishughulisha na mambo ya majirani zake, na bado akatumia fursa hio kuwasengenya. Mwingine huenda anajionyesha kuwa mtu mnyofu, lakini bado yuko tayari kuchukua pesa za mtu mwingine, maadamu asigunduliwe katika tendo hilo. Huenda atajaribu kujiaminisha binafsi  kwamba anaishi maisha ya juu kitabia kuliko watu wengine wakati yeye ni mdanganyifu. Mtu aliye na tabia hizi ni mnafiki wala si mwaminifu.

Unafiki wa wanadamu kila wakati ni kitu cha kumhuzunisha Mungu. Yesu asema, “Watu hawa huniheshimu kwa midomo; Ila mioyo yao iko mbali nami” (Mathayo 15:8). Changamoto kubwa kwa mwanadamu ni kuweka mdomo na moyo kwa pamoja. Uaminifu kutoka ndani yetu ndio ufunguo wa kupata neema na fadhili kwa Bwana.

Mkristo wa kweli ni mfano wa uaminifu. Kustawi kwake kiroho huendana na unyofu wake mbele ya Mungu. Uaminifu kwa binadamu wenzetu pia ni muhimu na unahitaji usikivu wa umakini. Katika maneno yetu, matendo ya shughuli zetu, na hata makubaliano ya kibiashara ni lazima tuhifadhi imani kwa watu wote. Ili tutende hili, ni lazima tuwe tayari kupata hasara kwa ajili ya ukweli.

Kuna somo tunaloweza kujifunza kutokana na simulizi hii. Mwalimu alimwuliza kijana mmoja swali:

“Je, ungesema uongo ukilipwa shilingi 50?”

“La hasha, mama” kijana akamjibu.

“Je, ungeweza kusema uongo ukilipwa shilingi elfu mbili?”

“La hasha, mama” kijana akamjibu.

“Je, ungeweza kusema uongo ukilipwa shilingi milioni mbili?”

“Lo!” akajisemea moyoni. “Ni kitu gani nisichoweza kukifanya nikiwa na shilingi milioni mbili?”

Wakati akisitasita, kijana mwingine nyuma yake akasema, “La hasha, mama”.

“Ni kwa nini?” mwalimu akauliza.

“Kwa sababu uongo unashikamana na mtu. Wakati hio hela zitakapoisha, na vitu vyote vizuri vilivyonunuliwa na pesa hizo vimetoweka, UONGO utabakia pale pale ulipo.”

Ukweli una umuhimu kiasi kwamba tungekuwa tayari kusumbukiwa kwa ajili yake. Sisi tukiwa tayari kusema uongo ili tujiokoe kutoka kwa kuaibishwa kwa muda mfupi, ni gharama kubwa mno kulipa kwa ajili ya kupotewa na uadilifu wetu. Pesa zipatikanazo kwa njia ya ujanja ni malipo duni kwa kujipatia dhamiri iliyonajisika, na hukumu ya milele ya Mungu inayokuja.

Je, wasema kwamba unatembea katika nuru ya Mungu na wakati huo huo unayatenda matendo maovu kama:

  • Unakataa kumsamehe ndugu au dada yako?
  • Hufanyi mapatano unapomtendea mtu vibaya?
  • Unatia chumvi kwenye ukweli?
  • Unavunja ahadi zako?
  • Unamwibia Mungu sadaka na zaka zake?
     

Uaminifu ni mtihani wa moyo. Mungu anafahamu mioyo yetu, na hakuna kitu kilichositirika kwake. Walakini wakati mwingine hatuwezi kumwambia Mungu kwa kadiri anavyotujua na jinsi tunavyojihisi ndani mwetu. Huenda hatuwaonyeshi jinsi ndivyo tulivyo kwa watu wengine. Mtu wa kweli mwenye furaha ni yule aliye mwaminifu mbele za Mungu, na anajikubali na kukiri jinsi alivyo. Na tukifungua mioyo na maisha yetu kwa Mungu, matatizo haya yote yanatatuliwa.

Malengo na misimamo yetu yanahitaji kuwasilishwa kwenye kipimo cha uaminifu. Kufaulu mtihani huu katika matendo yetu kwa Mungu na wanadamu, twahitaji mabadiliko ya ndani ya moyo, kwa maana mambo ya nje yanafafanua utu wetu wa ndani. Je, wewe ni mwaminifu? Mungu anatudai unyofu, watu wengine wote wanautegemea, na sisi wenyewe tutanufaika kwa kuushika. Ndiyo maisha yaliyo na thamani. “Tuna hakika kuwa tunayo dhamiri safi na shauku ya kuishi kwa uadilifu kwa kila njia.” (Waebrania 13:18 Tafsiri la NENO). Soma pia Mambo ya Walawi 19:35-36 na Mithali 19:5.

Mawasiliano

Kuagiza Vipeperushi

Hamna Budi Kuzaliwa Mara ya Pili

Yesu anatuambia kwamba milango ya mbinguni imefungwa dhidi yetu isipokuwa tunazaliwa mara ya pili. Kwa hiyo twauliza: “Rafiki, umezaliwa mara ya pili?” “Muumini wa kanisa, umezaliwa mara ya pili?” Ikiwa hapana, basi umepotea. Kwa maana Yesu anasema, “Mtu asipozaliwa mara ya pili, hawezi kuuona ufalme wa Mungu” (Yohana 3:3). Kwa kweli hakuna mtu anayetaka kufa akiwa mwenye dhambi, au kupotea; basi hamna budi kuzaliwa mara ya pili.

Unaweza ukauliza, “Kuzaliwa mara ya pili maana yake ni nini?” Leo, kuna mafundisho mengi ya uongo kuhusu kuzaliwa mara ya pili. Siyo ubatizo, kwa kuwa wengine walibatizwa na bado hawajazaliwa mara ya pili (Matendo 8:9-25). Siyo kujiunga na kanisa, kwa sababu wengine waliingia ndani kwa siri bila kufahamika (Wagalatia 2:4). Siyo kula meza ya Bwana, kwa maana baadhi walikula isiyostahili na iliwaletea hukumu (1Wakorintho 11:29). Siyo kubadilika au kujaribu kuishi maisha bora, “kwa maana nawaambia ya kwamba wengi watataka kuingia, wasiweze” (Luka 13:24). Siyo kusali, kwa maana Yesu asema, “Watu hawa huniheshimu kwa midomo; ila mioyo yao iko mbali nami” (Mathayo 15:8).

Mtu mwingine anaweza akasema, “Nikijaribu kuyafanya yote niwezayo: kuwapa maskini, kuwatembelea wagonjwa na kuwa mwema kila siku kadiri niwezavyo, basi kwa kweli nimezaliwa mara ya pili.” La, hasha, hatuwezi kuwa tofauti na jinsi tulivyo moyoni. “Kwa kuwa ile nia ya mwili ni uadui juu ya Mungu, kwa maana haitii sheria ya Mungu wala haiwezi kuitii” (Warumi 8:7). “Mti mwema hauwezi kuzaa matunda mabaya, wala mti mwovu kuzaa matunda mazuri.” (Mathayo 7:18) Tunapaswa kuwa na moyo uliobadilika. Kwa kuwa Mungu kupitia manabii, asema hivi, “Nami nitawapa ninyi moyo mpya, nami nitatia roho mpya ndani yenu, nami nitatoa moyo wa jiwe uliomo ndani ya mwili wenu, nami nitawapa moyo wa nyama” (Ezekieli 36:26).

Hivyo basi, kuzaliwa upya maana yake nini?” Kiini cha kuzaliwa upya ni kuwa na mabadiliko ya moyo kutoka kwa maisha ya kujitumikia kibinafsi, na kupata maisha ya kumtumikia Bwana. Mabadiliko haya hutokea wakati tunapojutia dhambi zetu, na kwa imani tukamtazamia Yesu kwa kuomba msamaha. Mtoto azaliwapo, uhai mpya unatokea, binadamu mpya katika mwili. Hali kadhalika, tunapozaliwa upya kwa roho, uhai mpya huu hutokea ambao ni ndani ya Yesu Kristo na unaongozwa na Roho Mtakatifu. Hivyo basi, kunaitwa kuzaliwa: uhai mpya ndani ya Kristo Yesu. “Bwana hakawii kuitimiza ahadi yaki, kama wengine wanavyokudhani kukawia, bali huvumilia kwenu, maana hapendi mtu ye yote apotee, bali wote wafikilie toba (2Petro 3:9).

Maandiko kamili ya: Hamna Budi Kuzaliwa Mara ya Pili

“Ni lini nitegemee kuzaliwa mara ya pili?” Maandiko matakatifu yasema, “Leo, kama mtaisikia sauti yake,” (Waebrania 3:7). Hii inamaanisha kwamba katika umri wowote, wakati wowote, au mahali popote, ukisikia mwito wake na kuitika unaweza ukazaliwa kwa mara ya pili kwa njia ya Roho.

“Itachukua muda gani? Si nitakua taratibu katika kuzaliwa upya?” La, tunazaliwa kwanza katika ufalme wa Mungu na kunatufanya tuwe wana na warithi. “na kama tu watoto, basi, tu warithi; warithi wa Mungu, warithio pamoja na Kristo” (Warumi 8:17). Kuzaliwa mara ya pili kunaweza kutokea mara moja unapomtolea Yesu vyote na kumwendea kupata msamaha.

“Kwa njia gani na lini ninaweza kuupokea?” Mungu anayechunguza moyo, aona uaminifu wako. Anakujia kupitia nguvu ya Roho Mtakatifu, na kuumbia moyoni mwako roho wa kweli. (Zaburi 51:10) Kwa njia hii unazaliwa upya- kiumbe kipya katika Kristo Yesu kwa kuwa na imani kwake. (2Wakorintho 5:17).

Hatimaye: “Kwa jinsi gani naweza kufahamu kwamba nimezaliwa upya tayari?” Paulo katika Warumi 8:1-10 anafundisha; “Lakini mtu awaye yote asipokuwa na Roho wa Kristo, huyo sio wake”. Biblia yafundisha kwamba waliopotea wamekufa dhambini, wamelaaniwa, na wana dhamiri iliyo ya uovu. Wana mawazo yenye tamaa ya kimwili, wasio na tumaini, wasiotii, na wasio na Mungu ulimwenguni. Lakini Mkristo aliyezaliwa mara ya pili ni mtoto wa Mungu, yu hai katika Kristo, ameokolewa, hana hatia ya dhambi, na anayo dhamiri safi. Naye anayo nia ya kiroho, amejazwa na Roho Mtakatifu na imani, na analo tumaini la uzima wa milele. Dhambi zake zimeondolewa kwa damu ya Yesu Kristo. Moyo wake umejazwa na upendo na amani wa Mungu zinazozidi ufahamu wote. Anayapenda mapenzi ya Bwana, na anayo shauku na amepewa uwezo kuyafanya mapenzi hayo. Pia anatembea na tumaini la uzima ng’ambo ya kaburi, na anayo ahadi ya makao yaliyopo mbinguni. Je, mtu anaweza kupata mageuzi kama haya na asiyatambue? La, hasha kwani “Roho mwenyewe hushuhudia pamoja na roho zetu ya kuwa sisi tu watoto wa Mungu” (Warumi 8:16). Ikiwa hujapata mabadiliko haya yaletayo amani na furaha moyoni, usipuuze, mtafute Mungu kwa moyo mmoja; kwa kuwa ni roho yako mwenyewe. Ni lazima uzaliwe mara ya pili.

Mawasiliano

Kuagiza Vipeperushi